Serikali
 imeanza kupanga walimu wa sayansi moja kwa moja katika shule badala ya 
Halmashauri kama ilivyokuwa awali ili kuleta uwiano sawa wa walimu 
katika shule mbalimbali nchini.
Hayo
 yamebainishwa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Suleman
 Jaffo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Muleba Prof. Anna Tibaijuka 
lililohusu mkakati wa Serikali katika kukabiliana na tatizo la upungufu 
wa walimu.
Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa
 Serikali imeandaa mkakati wa kuwaajiri wahitimu wa shahada za sayansi 
ambazo siyo za ualimu baada ya kuwapa mafunzo ya muda mfupi kuhusu mbinu
 za ufundishaji na maadili ya ualimu ili kukabiliana na changamoto ya 
walimu wa sayansi nchini.
Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa tayari kibali kimeombwa katika Ofisi ya Rais Utumishi kwa ajili ya utekelezaji huo, ambapo Serikali
 imepanga kuajiri walimu wastaafu wenye uwezo wa kufundisha waliokuwa 
wanafundisha masomo ya sayansi kwa mkataba ili kupunguza pengo lililopo.
Aidha,
 Naibu Waziri Jaffo amebainisha kuwa Serikali inafanya tathimini ya 
mahitaji ya walimu wa masomo ya sanaa kwa kila Halmashauri ili kubaini 
maeneo yenye ziada na yenye upungufu ili kusawazisha.
“Mpango
 wa Serikali uliopo ni kuwahamasisha walimu wa ziada wa masomo ya sanaa 
kwenda kufundisha katika shule za msingi ndani ya Halmashauri husika, 
ambapo kabla ya kuanza utekelezaji wa mabadiliko haya Serikali itatoa 
waraka maalumu kwenda katika Halmashauri zote nchini” amefafanua Naibu Waziri huyo.
Akizungumzia
 kuhusu utaratibu wa mafunzo ya walimu Mhe. Jaffo amesema kuwa 
Halmashauri moja haiwezi kuwa na mfumo wa peke yake wa kuandaa walimu 
hali ambayo iltakuwa ni vigumu kuthibiti ubora wa mafunzo hayo kwa 
walimu.
Hata
 hivyo amesema kuwa Serikali itaendelea kuongeza udahili wa walimu wa 
sayansi katika vyuo vya ualimu kadri watakavyojitokeza ili kukidhi 
mahitaji yaliyopo
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
