Wananchi
 wameaswa kuwa wavumilivu na kuendelea kushirikiana na Serikali wakati 
jitihada mbalimbali zikiendelea kuchukuliwa katika kukabiliana na athari
 za tetemeko la ardhi lililotokea Mkoani Kagera hivi karibuni.
Hayo
 yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) George 
Simbachawene alipokuwa akitoa kauli ya Serikali bungeni kuhusu Maafa 
yaliyosababishwa na tetemeko la ardhi lililotokea Mkoani Kagera siku ya 
jumamosi tarehe 10/09/2016.
Waziri
 Simbachawene amesema kuwa hadi leo tarehe 13/9/2016 idadi ya vifo 
vilivyosababishwa na tetemeko hilo katika Mkoa wa Kagera ni 17, ambapo 
majeruhi waliolazwa katika hospitali mbalimbali zilizoko Mkoani humo ni 
169, majeruhi waliotibiwa na kuruhusiwa ni 83, nyumba za makazi 
zilizoanguka ni 840, nyumba za makazi zenye nyufa ni 1,264 pamoja na 
taasisi zilizoanguka na kupata nyufa ni 44.
Aidha,
 Waziri Simbachawene amesema kuwa mpaka sasa Serikali imechukua hatua za
 kuwaokoa watu na kuwapeleka hospitali kwa ajili ya matibabu na 
kuwapatia makazi ya muda baadhi ya wananchi ambao nyumba zao 
zimeathirika.
Pia
 Serikali inaendelea kutibu majeruhi bure na wenye Bima za Afya kutumia 
bima zao na kuongeza nguvu ya madaktari bingwa 15 kutoka mkoa ya Mwanza 
ili kuweza kutoa huduma ya haraka kwa wahanga hao.
Vilevile
 Waziri Simbachawene amesema kuwa Serikali imeelekeza wanajiolojia 
kuwatoa hofu wananchi kwa kutoa maelekezo ya kisayansi kuhusu hali hiyo 
na kuendelea kufanya tahimini ya athari zilizosababishwa na tetemeko 
hilo.
Hata
 hivyo Waziri Simbachawene amesema kuwa serikali imezifunga shule za 
sekondari Ihungo na Nyakato zilizopo mkoani humo kutokana na athari za 
tetemeko iliyopelekea kuharibika kwa miundombinu ikiwemo madarasa, vyoo,
 mabweni na maabara, wakati serikali ikiendelea na taratibu za 
kushughulikia tatizo hilo.
Waziri
 Simbachawene ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa hatua 
za dharura zinachukuliwa kwa kushirikiana na wadau wengine ili 
kuhakikisha ili kuwasaidia wahanga.
Mbali
 na hayo Mbunge wa Mlalo Mhe. Rashid Shangazi ametoa hoja juu ya wabunge
 kuchangia posho yao ya siku moja ili iweze kuwasaidia wahanga wa 
tetemeko hilo lililokadiriwa kuwa na ukubwa wa kiwango cha 5.7 katika 
vipimo vya Richter ambapo wabunge waliunga mkono hoja hiyo na kuridhia 
kuchangia kusaidia maafa hayo.
Aidha,
 Mbunge wa Muleba, Prof. Anna Tibaijuka ameishukuru Serikali kuwepo 
kwenye eneo la tukio mkoani Bukoba hatua ambayo imewapa faraja 
wanakagera na kutoa wito kwa wabunge na watu wenye mapenzi mema kuzidi 
kuwafariji wahanga hao.
Kwa
 upande wake Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Charles Tizeba amesema 
kuwa Serikali itafanya tathmini ya kina na ya kitaalamu ili kuepuka wale
 ambao wanatumia maafa hayo katika kujinufaisha.
Akishukuru
 kwa niaba ya Serikali Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi 
William Lukuvi amewashukuru wadau wote kwa kujitokeza na kushirikiana na
 Serikali katika kutatua changamoto na kuwahakikishia wabunge kuwa 
mchango wao utawafika walengwa na kuongeza kuwa jambo hilo limepelekea 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kusitisha safari yake nchini 
Zambia ili kuweza kusimamia suala hilo.
Aidha,
 Waziri Lukuvi amesema kuwa Serikali inauchungu mkubwa juu ya maafa 
hayo, hivyo amewataka wadau mbalimbali kujitokeza kusaidiana na Serikali
 ili kuweza kuwasaidia wahanga hao  na kuwapa pole waathirika wa 
tetemeko hilo na kuwaombea marehemu wapumnzike kwa amani.  
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
