Featured
Loading...

Mugabe aonekana hadharani kwa mara ya kwanza toka Jeshi liingie Ikulu

Rais Robert Mugabe ameonekana hadharani kwa mara ya kwanza tangu jeshi lilipomweka chini ya kizuizi cha nyumbani baada ya leo kuhudhuria mahafali ya chuo kikuu.

Akiwa amevalia joho la kisomi lenye rangi za bluu na njano na kofia, Mugabe mwenye umri wa miaka 93 alikaa kwenye kiti mbele kabisa kwenye ukumbi na alishangiliwa kwa mbinja na vigelegele alipotangaza kwamba mahafali yamefunguliwa.

Mkongwe huyo aliyetawala Zimbabwe tangu ilipopata uhuru mwaka 1980, kwanza akiwa waziri mkuu (1980 hadi 1987) na baadaye rais (1987 hadi sasa) aliwekwa chini ya kizuizi cha nyumbani kwake kuanzia Jumanne ikiwa ni wiki moja baada ya kumfuta kazi aliyekuwa makamu wake wa rais Emmerson Mnangagwa.

Hatua ya kumfukuza kazi Mnangagwa ilichukuliwa na wengi kwamba ulikuwa mpango wa kumpandisha mkewe, Grace katika nafasi hiyo ya makamu wa rais na hivyo kumtengenezea mazingira ya kurithi urais wa mumewe.

Zimbabwe ilibaki imeduwaa baada ya jeshi kuingilia kati katikati ya mzozo mkali wa kuwania uongozi wa nchi kati ya Grace na Mnangagwa, 75.

Wachambuzi wa masuala ya siasa wanasema kwamba jeshi linapinga Grace kupanda hadi kuwa kiongozi wakati Mnangagwa ndiye mwenye uhusiano mzuri na jeshi hilo.

Mugabe na wakuu wa jeshi wamekutana kwa mazungumzo na hatua yao ya kunyakua madaraka ni ishara kwamba mkongwe huyo anaondoka.
Mnangagwa, ambaye anapewa nafasi kubwa ya kuwa kiongozi mpya amerejea nchini baada ya kutoroka nchi akihofia usalama wake. Jeshi limesema kuwa lilikuwa katika mazungumzo na Mugabe na litaujulisha umma kuhusu matokeo ya mazungumzo hayo haraka iwezekanavyo.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top