ACT Wazalendo Kutoshiriki Uchaguzi wa Marudio wa Tarehe 13 Januari 2017
Jana,
Disemba 16, 2017, Kamati Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo ilifanya kikao
chake cha dharura jijini Dar es salaam, lengo likiwa ni kujadili hali ya
kisiasa ndani na nje ya Chama, Hali ya Uchumi wa Nchi, kupokea taarifa
juu ya mwenendo wa Chaguzi ndogo katika Kata 43 nchini uliofanyika
Novemba 26, 2017, pamoja na kutoa uamuzi juu ya ushiriki wa Chama katika
chaguzi ndogo zilizotangazwa karibuni na tume ya uchaguzi nchini (NEC)
na kutarajiwa kufanyika Januari 13, 2018.
A: Hali ya Nchi (Kisiasa na Kiuchumi)
Kamati
Kuu ilijadili mwenendo wa matukio tangu ilipotoa taarifa yake juu ya
kuisnyaa kwa uchumi wa nchi pamoja na taarifa za takwimu za Serikali.
Tangu kukamatwa kwa Kiongozi wa Chama, kuhojiwa kwa Mwenyekiti wa Chama
Taifa, kuhojiwa kwa Katibu Mkuu wa Chama, Kuzuiwa kwa simu ya Kiongozi
wa Chama, pamoja na Kompyuta za Chama pamoja na wito wa kutaka kuihoji
Kamati Kuu nzima ya Chama kwa sababu ya taarifa yake juu ya takwimu za
Serikali. Kamati Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo inapinga unyanyasaji
unaofanyika dhidi yetu kwa sababu tu ya chama chetu kuzungumzia masuala
ya Uchumi wa nchi unaosinyaa.
Juzi,
Disemba 13, 2017 Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limeitaka Serikali
itazame upya vyanzo vyake vya takwimu za uchumi ili kupata picha halisi
ya Hali ya uchumi wa Taifa letu. IMF wamethibitisha kuwa ukuaji wa
uchumi wa Tanzania unashuka (unasinyaa) kutoka 7.2% mpaka 6.8%, na
kwamba Takwimu za Serikali ni lazima zitazamwe upya. Jambo ambalo sisi
ACT Wazalendo tulilisema kabla.
Jeshi
letu la Polisi halijavamia Ofisi za IMF na kumuweka ndani Mkurugenzi
wake mkazi hapa nchini, inasikitisha kwamba Serikali inawasikiliza na
kuheshimu zaidi maoni ya kiuchumi ya IMF kuliko yanayotolewa na
Watanzania. Maoni kama ya IMF yalipotolewa na ACT Wazalendo
yalisababisha unyanyasaji mkubwa kwa Viongozi wetu. Tunatarajia kuwa
Jeshi la Polisi litarudisha vifaa vyote vya chama lilivyo navyo, na
kutuacha kuendelea na uchambuzi wa shughuli za Serikali kwa uhuru.
Jambo
moja muhimu ambalo watu wa IMF wameiambia Serikali ni suala la
kuheshimu Bajeti. Mtakumbuka tulieleza katika kikao kilichopita kuwa
Serikali ya Awamu ya Tano imeanza tabia ya kutumia fedha za Mashirika ya
Umma bila kufuata taratibu za sheria. Kwa mfano mapema katika mwaka wa
fedha 2016/17, Serikali ilipata gawio la shilingi bilioni 300 kutoka
Benki Kuu ya Tanzania (BOT) kutokana na faida ya benki hiyo mwaka
2015/16. Taarifa juu ya gawio hilo inapatikana katika wavuti ya BOT.
Kinyume
na utaratibu, Serikali haikutoa taarifa juu ya gawio hili popote kwenye
taarifa zake za kiFedha. Mapato haya hayakupelekwa Bungeni kugawiwa kwa
mujibu wa sheria. Taarifa ni kuwa Serikali iliamua kutumia fedha hizi
kulipia Mkandarasi wa Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Chato, pamoja na
madeni ya ndege za Bombardier na Boeing bila kufuata taratibu za sheria
za fedha na bila Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, CAG
kuidhinisha kwa mujibu wa Katiba. Utaratibu unataka fedha kuingia kwenye
Mfuko Mkuu (Consolidated Fund) na kisha kuidhinishwa na CAG, na ndipo
Serikali kuanza kutumia.
Shilingi
bilioni 300 kutumika na Serikali bila kushirikisha Bunge na kufuata
sheria za nchi ni kusigina Katiba na kudharau Taasisi za Uwajibikaji za
nchi. Kamati Kuu inamtaka CAG afanye ukaguzi maalumu wa fedha hizi na
kutoa taarifa kwa Bunge, ili Bunge lichukue hatua za kuiwajibisha na
kuisimamia Serikali ipasavyo.
Kamati
Kuu pia ilipokea taarifa juu ya hali ya usalama nchini, hasa juu ya
mwenendo wa watu kupotea katika mazingira ya kutatanisha. Tukio la
karibuni likiwa ni kupotea kwa Mwandishi wa magazeti ya Kampuni ya
Mwananchi Communications, ndugu Azory, mwandishi wa habari za uchunguzi,
hasa wa eneo la Kibiti. Tunaungana na Familia yake, waandishi wenzake,
wa ndani na Nje ya Nchi, pamoja na Watanzania wote, kulitaka Jeshi la
Polisi kuhakikisha Azory anapatikana akiwa hai.
B: Nafasi ya Chama chetu juu ya Miswada inayokwenda Bungeni mwaka 2018
Moja
ya ajenda kubwa ya Chama chetu ni Hifadhi ya jamii. Chama chetu
kinataka haki ya hifadhi ya jamii kwa kila raia ili kuwa na Taifa ambalo
raia wake wote wana bima ya afya na uhakika wa pensheni uzeeni. Katika
ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu tuliahidi mabadiliko makubwa ya mfumo
wa hifadhi ya jamii ikiwemo kuunganisha mifuko iliyopo na kubakia na
mifuko 3 tu. Mifuko miwili ya pensheni, na mfuko mmoja ni mfuko wa Taifa
wa bima ya afya.
Serikali
imeamua kutekeleza wazo letu hilo na tayari muswada wa sheria ya
hifadhi ya jamii umewasilishwa bungeni kwa ajili ya kuanza kufanyiwa
kazi na kuunda mifuko miwili tu. Tunapongeza hatua hii ya Serikali
kuchukua mawazo yetu na kuyafanyia kazi, japo utekelezaji wake
unafanyika vibaya, na hivyo utashindwa kuleta mafanikio tarajiwa. Kamati
Kuu imeona hatua ya Serikali kuimarisha sekta ya hifadhi ya jamii kwa
Wafanyakazi wa sekta rasmi, lakini imesikitishwa na hatua ya Serikali
hiyo hiyo kutochukua nafasi hii kuweka mazingira wezeshi ya kisheria kwa
Wakulima, Wafugaji, Wavuvi na wote walio katika Sekta isiyo rasmi
kuingia kwenye Hifadhi ya Jamii.
Kamati
Kuu ya ACT Wazalendo pia imeona kuwa muswada huu unaopendekezwa bungeni
una matatizo makubwa ambayo yanaweza kusababisha wazee wetu 120,000
kukosa kabisa pensheni, hasa watakaoanza kustaafu mwaka huu na
waliokwishastaafu tangu mwaka 1999.
Jambo
hili ni la kihistoria kidogo, tutaeleza. Serikali mwaka 1999 iliunda
Mfuko wa PSPF kwa ajili ya watumishi wa umma. Kabla ya mwaka 1999
Watumishi wa Umma walikuwa hawachangii pensheni zao, bali walikuwa
wanalipwa pensheni kutoka Hazina moja kwa moja kupitia bajeti za
Serikali za kila mwaka. Hii ndio sababu wastaafu wetu nchini wanapokea
pensheni ndogo sana ya shilingi 50,000 tu kwa mwezi na kabla ya hapo
shilingi 20,000 tu.
Serikali
ya Awamu ya 3 iliamua kuunda Mfuko wa Pensheni ili kuboresha pensheni
za watumishi wa umma. Hata hivyo, Serikali ilitakiwa kulipa michango ya
wafanyakazi wote walioajiriwa kabla ya mwaka 1999 (pre 1999). Serikali
ya Rais Mkapa ilikubali deni lakini haikulipa. Serikali ya Rais Kikwete
ilifanya uhakiki wa Deni na kukubali kulipa lakini haikulipa. Serikali
ya Rais Magufuli imeamua kutolipa kabisa kisheria. Taarifa ni kuwa
Serikali imeamua kuachana na madeni haya, na hivyo wastaafu 120,000
nchini wako hatarini kutolipwa pensheni kabisa, mara tu baada ya muswada
huu mpya kupita na kuwa sheria.
Vile
vile muswada wa sheria hii unabadilisha kanuni ya mafao, na hivyo
kuathiri Wafanyakazi wa Umma hususan Walimu wetu wote nchi nzima ambapo
pensheni zao zitakatwa kwa 50%. Jambo hilo litakuwa na athari kubwa mno
kwa walimu nchini.
Muswada
pia umeshindwa kuwaka bayana jawabu la kujitoa kwenye mafao kupitia
kinachoitwa 'Fao la Kujitoa'. Muswada umeweka mamlaka ya fao jipya la
kukosa ajira kwa Waziri badala ya kuweka masharti yake wazi kisheria na
hivyo kuendeleza utata wa suala zima la wafanyakazi na michango yao.
Muswada pia umeendelea na kiwango cha michango cha 20% licha ya tafiti
zote kuonyesha kuwa ni kiwango kikubwa mno na kinaweza kupunguzwa mpaka
12% ambapo Waajiri wachangie 7% na waajiriwa 5% ya mishahara yao kwa
mwezi kwenye mifuko ya hifadhi ya Jamii.
Muswada
pia umeshindwa kuunganisha Michango kwenye mifuko na Fao la Matibabu
kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Hali ya sasa ni kwamba
wafanyakazi wanalipa mara mbili, wanalipia pensheni kwenye mifuko ya
pensheni, na wanalipoa NHIF kwaajili ya Bima ya Afya. Wakati Fao la Afya
ni kitu kinachopaswa kuwa sehemu ya faida za mafao ya kuingia kwenye
Hifadhi ya Jamii.
Kamati
Kuu imeiagiza Sekretarieti ya Chama kuanza kazi ya kuhamasisha makundi
ya vyama vya Wafanyakazi nchini kuungana na kusimama pamoja kuboresha
muswada wa Sheria hii. Lengo likiwa muswada huu usiende Bungeni ili
uboreshwe na kulinda maslahi ya wazee wetu wastaafu na wastaafu wajao.
Kamati
Kuu imeagiza Chama kuitisha kongamano la wazi kuvileta pamoja vyama vya
wafanyakazi, wafanyakazi wenyewe na wadau wengine muhimu ili kujadili
sheria mpya ya pensheni na kujiunga na vyama vya wafanyakazi kuboresha
muswada ili kutunga sheria inayohakikisha kuwa kila Mtanzania anakuwa na
haki ya Hifadhi ya jamii.
Muswada
mwengine ni muswada wa Sheria Mpya ya Vyama vya Siasa nchini, miongoni
mwa miswada mibaya zaidi kuwahi kutokea nchini, muswada ambao ukiachwa
kama ulivyo na ukawa sheria basi utafuta siasa za vyama vingi nchini.
Maana
ni muswada unaompa Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini mamlaka ya
Udhibiti na Uendeshaji wa Vyama na kupoka mamlaka hayo kwa Vyama
vyenyewe kupitia wanachama. Hata zuio haramu la mikutano ya hadhara
nchini limewekwa kisheria katika mswada huo.
Kamati
Kuu imeiagiza Sekretarieti ya Chama kuanzisha mara moja mazungumzo na
Vyama vingine vya upinzani ili kuunganisha nguvu kuupinga muswada huu
unaokwenda kurudisha nchi kwenye mfumo wa Chama kimoja cha siasa.
C: Ushiriki wa Chama Kwenye Uchaguzi wa Marudio wa Januari 13, 2018
Kamati
Kuu ilijadili na kutathmini kwa kina yaliyojitokeza kwenye uchaguzi wa
Novemba 2017. Kwenye uchaguzi huo, ilikuwa dhahiri kuwa;
I.
Chama Tawala na Serikali yake kiliongeza matumizi ya mabavu kupitia
vyombo vya dola hasa jeshi la polisi ili kuweka mazingira ya kushinda
uchaguzi
II.
Chama Tawala kilihakikisha kinawatumia vyema watendaji wa halmashari
wanaohusika na usimamizi wa uchaguzi ambao wengi waliteuliwa kwa misingi
ya ukada kwa Chama hicho ili kujihakikishia ushindi.
III.
Mazingira yalipoonekana dhahiri kuwaelemea, Chama Tawala walitumia njia
za kimabavu Kama vile kuvamia viongozi, kuteka viongozi, au kuwaweka
mahabusu viongozi na mawakala
IV.
Kila mbinu ilipoonekana kugonga mwamba, kwenye maeneo kadhaa, Chama
Tawala, kwa kutumia vyombo vya dola kiliamua kujitangazia ushindi
kimabavu licha ya matokeo kuonesha kuwa wameshindwa
V.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi, NEC ilionekana kutojali kabisa hitilafu
zilizojitokeza na kuchukua hatua kurekebisha kabla ya kuitisha Uchaguzi
Mpya.
Kutokana
na vitendo hivyo, ni dhahiri kwamba uwanja wa demokrasia nchini
umevurugwa sana na mchakato mzima wa uchaguzi huru na wa haki kuharibiwa
kabisa. Hivyo basi, Kamati Kuu ya Chama chetu imeazimia kuwa Chama
chetu KISISHIRIKI kwenye uchaguzi ujao wa marudio wa tarehe 13 Januari
2018.
Hata
hivyo tunatambua kuwa kutoshiriki chaguzi tu haitoshi kwani haijibu
swali la nini kinafuata baada ya kususia. Chama pia kinatambua kuwa
Chama tawala kinafurahia kususiwa na kuna uwezekano mkubwa wa kuendelea
kubinya Demokrasia ili Vyama vya upinzani viendelee kususia chaguzi
zinazokuja.
Kamati
Kuu imeuagiza Uongozi wa Taifa wa Chama kuwafikia wadau wote wa
Demokrasia nchini na kuweka mikakati ya pamoja ya hatua za ziada za
kuchukua ili kuboresha mazingira ya chaguzi za haki nchini kwetu, pamoja
na kuweka shinikizo kubwa kwa Serikali kufanya mabadiliko muhimu ya
kisheria, kiutendaji na kikatiba ili kuweka sawa uwanja wa mapambano ya
Kidemokrasia.
Chama
chetu kitavitembela na kuanzisha mazungumzo na Vyama vyote vya upinzani
ili kuona njia bora zaidi ya kimapambano ya pamoja katika kukabiliana
na vitendo vya sasa vya Chama Tawala cha kuvuruga uchaguzi huru na wa
haki.
Chama
pia kitautumia muda wa sasa na mwezi Januari Kama kipindi cha
kushirikiana na Vyama vya wafanyakazi na wafanyakazi wenyewe kupambana
dhidi ya Muswada wa Sheria ya Pensheni ambao utawakosesha pensheni
malaki ya wafanyakazi wa sekta ya umma hasa walimu kama utapitishwa kama
ulivyo. Hatua hizi pia zitahusisha makundi ya walio kwenye sekta isiyo
rasmi, kama wakulima, wavuvi, wamachinga, wajasiriamali nk, ambao sheria
hii inawaacha nje kabisa.
ACT Wazalendo
Disemba 17, 2017
Dar es Salaam
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )