Featured
Loading...

UKAWA Watishia Kususia Uchaguzi Jimbo la Nyalandu.....Watoa Masharti Tume ya Uchaguzi

Vyama  vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vimetishia kutoshiriki uchaguzi mdogo wa ubunge katika majimbo matatu, likiwamo la Singida Kaskazini la aliyekuwa mwakilishi Lazaro Nyalandu, endapo Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) haitotangaza kuuahirisha na kuupangia tarehe nyingine.

Hata hivyo, tume hiyo imesema itaendelea kutekeleza majukumu yake ikibainisha kuwa katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya kikatiba, haitalazimika kufuata amri au maagizo ya mtu yeyote au idara yoyote ya serikali au maoni ya chama chochote cha siasa.

Nyalandu, waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii, alitangaza kuachia ubunge wa Sindiga Kaskazini na kuihama CCM Oktoba 30, mwaka huu kisha kujiunga na Chadema kutokana na kile alichodai kutoridhishwa na mwenendo wa sasa wa chama tawala.

Ukawa umeitaka tume hiyo kuusogeza mbele uchaguzi huo ili kwanza kuwe na majadiliano baina ya tume, vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi kuepuka ilichodai kasoro zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mdogo wa madiwani wa kata 43 uliofanyika Novemba 26, mwaka huu.

Umoja huo unaundwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama cha Wananchi (CUF), NCCR-Mageuzi na NLD.

Hata hivyo, CUF kwa sasa imegawanyika katika makundi mawili - moja likimuunga mkono Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba na jingine likiwa upande wa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad.

Mapema mwezi huu, Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Hamid Mahmoud Hamid, alitangaza kuwa uchaguzi mdogo katika majimbo matatu ya Singida Kaskazini, Longido na Songea Mjini, na kata sita za Tanzania Bara utafanyika Januari 13.

Hata hivyo, zikiwa zimebaki siku 32 kabla ya kufanyika kwake, Ukawa jana ulitangaza tishio la kutoshirika katika uchaguzi huo endapo NEC haitauahirisha na kupanga tarehe nyingine na pia kutoa nafasi kwa vyama vyote na wadau husika kukaa pamoja kujadili na kuzipatia majibu "kasoro" zilijitokeza katika uchaguzi mdogo uliopita.

Ukawa umedai uchaguzi huo ambao chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilitangazwa mshindi katika kata 42 kati ya 43 zilizoshindaniwa, haukuwa huru na wa haki hivyo kuna haja kuitishwa mkutano wa wadau kutatua changamoto zilizojitokeza wakati wa uchaguzi huo na kuzitafutia utatuzi kabla ya kuingia kwenye uchaguzi mwingine.

Wakizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, viongozi wa Ukawa walidai tayari wameshaiandikia barua NEC kuomba uchaguzi huo usogezwe mbele igawa bado hawajajibiwa.

Katika mkutano huo na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Ukawa, Freeman Mbowe, akizungumza kwa niaba ya viongozi wenzake, alibainisha mambo kadhaa ambayo yamewalazimu waombe uchaguzi huo usogezwe mbele ikiwa ni pamoja na kutangaza uchaguzi katika Jimbo la Longido ilhali bado kuna kesi kwenye Mahakama ya Rufani inayolihusu.

"Jimbo la Longido Kaskazini kwa mujibu wa sheria za uchaguzi haliko wazi," Mbowe alisema, "bado halijaiva kwa ajili ya uchaguzi kwa sababu rufani yake bado iko mahakama ya rufani na imekatwa kwa kufuata utaratibu, inakuwaje utangaze uchaguzi wakati rufani imekatwa?"

Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Taifa na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni alisema sababu ya pili ni kasoro zilizojitokeza katika uchaguzi mdogo katika kata 43 mwezi uliopita, akidai kuwa pamoja na mambo mengine, NEC ilishindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo na kusababisha uchaguzi huo kutokuwa huru na wa haki.

Mbowe alisema sababu ya tatu iliyoulazimu Ukawa kuomba kusogezwa mbele kwa uchaguzi mdogo wa majimbo matatu ni kutumika kwa nguvu kubwa ya vyombo vya dola katika uchaguzi mdogo uliopita, huku wanachama, viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa na wabunge wakikamatwa ovyo.

“Tumeona umwagaji wa damu katika uchaguzi huo mdogo na mambo hayo yanafanyika ikiwamo kwa kutumia silaha za asili na za moto," Mbowe alisema na kueleza zaidi:

"Tumeona viongozi wa mikoa wakifanya kampeni na wakati mwingine kuwaamrisha polisi nini cha kufanya katika uchaguzi huo japokuwa hawaruhusiwi kufanya hivyo, wasimamizi wa uchaguzi nao hawakubaki nyuma, Nec wamejidhihirisha kushindwa kutekeleza wajibu wao.

“Katika nchi hii tukiendelea tunavyoendelea, hakuna uchaguzi utakaofanyika kwa kufuata sheria na kanuni zilizopo. Mazingira ambayo sheria haziheshimiwi, tukishajenga tabia hiyo hakutakuwa tena na uchaguzi huru."

'Kigogo' huyo wa Ukawa alidai kukimbia moja kwa moja kwenda katika uchaguzi katika mazingira hayo kunaweza kuleta mpasuko na pia umoja huo ukifanya hivyo, hautakuwa unalitendea haki taifa.

“Kwa mantiki hiyo, uchaguzi huo unastahili kuahirishwa," Mbowe alisema, "ni rai yetu kwa serikali na NEC kuona umuhimu wa kuahirisha kwanza uchaguzi huo ili wadau mbalimbali wa vyama vya siasa na washiriki wa shughuli hizo, kutafakari wamepata funzo gani katika uchaguzi wa kata 43.

"Kuna mazingira gani ya kufanya siasa katika nchi  yetu inayotupa 'justification‘ (uhalali) ya kwenda kwenye kufanya chaguzi, kuendelea kushiriki chaguzi za kuumiza watu, kufunga watu, za kuvunja amani, hazitujengi kama taifa isipokuwa tunaongeza mpasuko na ufa kati yetu.

“Kwa sisi, rai yetu kama viongozi wakuu wa kitaifa wa Ukawa ni kwamba, muda uliotolewa na kutangazwa uchaguzi huu bila kufanya ‘consultation’ (majadiliano) na vyama vya siasa japo NEC wanaweza kujitetea kwamba sheria inawapa mamlaka hayo, lakini tunaamini kwa upande wa pili uongozi ni pamoja na kusoma ‘between the line’ (kutafakari kwa makini) kwamba kuna viashiria vyote vya kupoteza amani katika taifa.

"Kwa hiyo, tunaiomba serikali chaguzi hizi zisogezwe mbele, wadau tukae kwanza, vyama vya siasa na wadau wengine tukae tuzungumze. Hivi kweli tumechagua uchaguzi ukawe ni wa mapanga, visu na rungu? Hivi kweli tumekubaliana kwamba mawakala watolewe vituoni?

“Na tukishakubaliana juu ya haya, maadili na kwanini yalikiukwa? Kwa sababu si kila jambo lazima liende mahakamani japo wao wanasema mkiona hamjaridhika muende mahakamani, ila wakumbuke kwamba mahakamani pia ni kuchelewesha haki na mambo ya kisiasa hayako hivyo.

"Ni vema wakaangalia namna uchaguzi huu uahirishwe ili wahusika wakae na kutafakari tulikotoka na tuliko na tunakotaka kwenda, kama Tume na serikali itapuuza rai yetu, sisi kama umoja wetu wa vyama hivi hatutakuwa tayari kushiriki uchaguzi huo."

Katibu Mkuu wa NLD, Toz Matwanga, aliyekuwa amefuatana na Mbowe kwenye mkutano huo, alisema sheria inavipa haki vyama vya siasa vyote kufanya siasa kwa amani, hivyo kuvinyima haki hiyo ni kosa.

Katika mkutano huo, mbali na Matwanga, Mbowe pia alifuatana na viongozi wa NCCR-Mageuzi na CUF kutoka upande wa Maalim Self.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top