Vyama
vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vimetishia kutoshiriki
uchaguzi mdogo wa ubunge katika majimbo matatu, likiwamo la Singida
Kaskazini la aliyekuwa mwakilishi Lazaro Nyalandu, endapo Tume ya Taifa
ya Uchaguzi (NEC) haitotangaza kuuahirisha na kuupangia tarehe nyingine.
Hata
hivyo, tume hiyo imesema itaendelea kutekeleza majukumu yake
ikibainisha kuwa katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti
ya kikatiba, haitalazimika kufuata amri au maagizo ya mtu yeyote au
idara yoyote ya serikali au maoni ya chama chochote cha siasa.
Nyalandu,
waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii, alitangaza kuachia ubunge wa
Sindiga Kaskazini na kuihama CCM Oktoba 30, mwaka huu kisha kujiunga na
Chadema kutokana na kile alichodai kutoridhishwa na mwenendo wa sasa wa
chama tawala.
Ukawa
umeitaka tume hiyo kuusogeza mbele uchaguzi huo ili kwanza kuwe na
majadiliano baina ya tume, vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi
kuepuka ilichodai kasoro zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mdogo wa
madiwani wa kata 43 uliofanyika Novemba 26, mwaka huu.
Umoja huo unaundwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama cha Wananchi (CUF), NCCR-Mageuzi na NLD.
Hata
hivyo, CUF kwa sasa imegawanyika katika makundi mawili - moja
likimuunga mkono Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba na
jingine likiwa upande wa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad.
Mapema
mwezi huu, Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Hamid Mahmoud Hamid,
alitangaza kuwa uchaguzi mdogo katika majimbo matatu ya Singida
Kaskazini, Longido na Songea Mjini, na kata sita za Tanzania Bara
utafanyika Januari 13.
Hata
hivyo, zikiwa zimebaki siku 32 kabla ya kufanyika kwake, Ukawa jana
ulitangaza tishio la kutoshirika katika uchaguzi huo endapo NEC
haitauahirisha na kupanga tarehe nyingine na pia kutoa nafasi kwa vyama
vyote na wadau husika kukaa pamoja kujadili na kuzipatia majibu "kasoro"
zilijitokeza katika uchaguzi mdogo uliopita.
Ukawa
umedai uchaguzi huo ambao chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM)
kilitangazwa mshindi katika kata 42 kati ya 43 zilizoshindaniwa, haukuwa
huru na wa haki hivyo kuna haja kuitishwa mkutano wa wadau kutatua
changamoto zilizojitokeza wakati wa uchaguzi huo na kuzitafutia utatuzi
kabla ya kuingia kwenye uchaguzi mwingine.
Wakizungumza
na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, viongozi wa Ukawa
walidai tayari wameshaiandikia barua NEC kuomba uchaguzi huo usogezwe
mbele igawa bado hawajajibiwa.
Katika
mkutano huo na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Ukawa, Freeman Mbowe,
akizungumza kwa niaba ya viongozi wenzake, alibainisha mambo kadhaa
ambayo yamewalazimu waombe uchaguzi huo usogezwe mbele ikiwa ni pamoja
na kutangaza uchaguzi katika Jimbo la Longido ilhali bado kuna kesi
kwenye Mahakama ya Rufani inayolihusu.
"Jimbo
la Longido Kaskazini kwa mujibu wa sheria za uchaguzi haliko wazi,"
Mbowe alisema, "bado halijaiva kwa ajili ya uchaguzi kwa sababu rufani
yake bado iko mahakama ya rufani na imekatwa kwa kufuata utaratibu,
inakuwaje utangaze uchaguzi wakati rufani imekatwa?"
Mbowe
ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Taifa na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya
Upinzani Bungeni alisema sababu ya pili ni kasoro zilizojitokeza katika
uchaguzi mdogo katika kata 43 mwezi uliopita, akidai kuwa pamoja na
mambo mengine, NEC ilishindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo na
kusababisha uchaguzi huo kutokuwa huru na wa haki.
Mbowe
alisema sababu ya tatu iliyoulazimu Ukawa kuomba kusogezwa mbele kwa
uchaguzi mdogo wa majimbo matatu ni kutumika kwa nguvu kubwa ya vyombo
vya dola katika uchaguzi mdogo uliopita, huku wanachama, viongozi
mbalimbali wa vyama vya siasa na wabunge wakikamatwa ovyo.
“Tumeona
umwagaji wa damu katika uchaguzi huo mdogo na mambo hayo yanafanyika
ikiwamo kwa kutumia silaha za asili na za moto," Mbowe alisema na
kueleza zaidi:
"Tumeona
viongozi wa mikoa wakifanya kampeni na wakati mwingine kuwaamrisha
polisi nini cha kufanya katika uchaguzi huo japokuwa hawaruhusiwi
kufanya hivyo, wasimamizi wa uchaguzi nao hawakubaki nyuma, Nec
wamejidhihirisha kushindwa kutekeleza wajibu wao.
“Katika
nchi hii tukiendelea tunavyoendelea, hakuna uchaguzi utakaofanyika kwa
kufuata sheria na kanuni zilizopo. Mazingira ambayo sheria
haziheshimiwi, tukishajenga tabia hiyo hakutakuwa tena na uchaguzi
huru."
'Kigogo'
huyo wa Ukawa alidai kukimbia moja kwa moja kwenda katika uchaguzi
katika mazingira hayo kunaweza kuleta mpasuko na pia umoja huo ukifanya
hivyo, hautakuwa unalitendea haki taifa.
“Kwa
mantiki hiyo, uchaguzi huo unastahili kuahirishwa," Mbowe alisema, "ni
rai yetu kwa serikali na NEC kuona umuhimu wa kuahirisha kwanza uchaguzi
huo ili wadau mbalimbali wa vyama vya siasa na washiriki wa shughuli
hizo, kutafakari wamepata funzo gani katika uchaguzi wa kata 43.
"Kuna
mazingira gani ya kufanya siasa katika nchi yetu inayotupa
'justification‘ (uhalali) ya kwenda kwenye kufanya chaguzi, kuendelea
kushiriki chaguzi za kuumiza watu, kufunga watu, za kuvunja amani,
hazitujengi kama taifa isipokuwa tunaongeza mpasuko na ufa kati yetu.
“Kwa
sisi, rai yetu kama viongozi wakuu wa kitaifa wa Ukawa ni kwamba, muda
uliotolewa na kutangazwa uchaguzi huu bila kufanya ‘consultation’
(majadiliano) na vyama vya siasa japo NEC wanaweza kujitetea kwamba
sheria inawapa mamlaka hayo, lakini tunaamini kwa upande wa pili uongozi
ni pamoja na kusoma ‘between the line’ (kutafakari kwa makini) kwamba
kuna viashiria vyote vya kupoteza amani katika taifa.
"Kwa
hiyo, tunaiomba serikali chaguzi hizi zisogezwe mbele, wadau tukae
kwanza, vyama vya siasa na wadau wengine tukae tuzungumze. Hivi kweli
tumechagua uchaguzi ukawe ni wa mapanga, visu na rungu? Hivi kweli
tumekubaliana kwamba mawakala watolewe vituoni?
“Na
tukishakubaliana juu ya haya, maadili na kwanini yalikiukwa? Kwa sababu
si kila jambo lazima liende mahakamani japo wao wanasema mkiona
hamjaridhika muende mahakamani, ila wakumbuke kwamba mahakamani pia ni
kuchelewesha haki na mambo ya kisiasa hayako hivyo.
"Ni
vema wakaangalia namna uchaguzi huu uahirishwe ili wahusika wakae na
kutafakari tulikotoka na tuliko na tunakotaka kwenda, kama Tume na
serikali itapuuza rai yetu, sisi kama umoja wetu wa vyama hivi
hatutakuwa tayari kushiriki uchaguzi huo."
Katibu
Mkuu wa NLD, Toz Matwanga, aliyekuwa amefuatana na Mbowe kwenye mkutano
huo, alisema sheria inavipa haki vyama vya siasa vyote kufanya siasa
kwa amani, hivyo kuvinyima haki hiyo ni kosa.
Katika mkutano huo, mbali na Matwanga, Mbowe pia alifuatana na viongozi wa NCCR-Mageuzi na CUF kutoka upande wa Maalim Self.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )