Featured
Loading...

TAMBWE 'MAGOLI' AIKATAA SIMBA



Mtangazaji wa Azam TV na mmiliki wa MPENJA BLOG, Baraka Adson Mpenja (kulia) akieleza kwa kifupi tathmini ya mechi ya Yanga v Coastal Union kabla ya kumhoji mfungaji wa magoli manne (4) kati ya 8, Amissi Tambwe

Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
'Tambwe ameifungia Simba SC mabao 21 katika Ligi Kuu Tanzania, 19 akiyafunga msimu uliopita na mawili msimu huu kabla ya kutimkia Yanga SC dirisha dogo.'
BAADA ya kuwa na wakati mzuri ndani ya kikosi cha Yanga SC, mshambuliaji Amisi Tambwe, amesema hafikirii kurejea mtaa wa Msimbazi jijini hapa kuitumikia kwa mara ya pili Simba SC.
Katika mahojiano na mtandao huu jijini hapa leo, Tambwe, mchezaji wa zamani wa Vital'O ya kwao Burundi, amesema anajisikia vyema kucheza ndani ya kikosi cha Mdachi Hans van der Pluijm cha Yanga SC.
Amesema taarifa zinazoenezwa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba ana mpango wa kurejea Simba SC baada ya msimu huu kumalizika si za kweli.
"Sifikirii kurudi Simba. Mimi ni mchezaji wa Yanga na ninajisikia vizuri kuwa hapa. Nimefunga magoli tisa ligi kuu na mawili katika michuano ya kimataifa. Ni jambo jema kwangu na klabu ya Yanga pia," amesema Tambwe.
Aidha, straika huyo ambaye msimu huu amefunga mabao saba kwa kichwa na manne kwa mguu (matatu mguu wa kulia) katika mashindano yote akiwa na Simba SC na Yanga SC, amesema mabao yake manne katika mechi ya jana yamerejesha matumaini kutetea kiatu chake cha dhabu cha zawadi ya mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Bara msimu huu.
Tambwe alifunga mabao manne Yanga ilipowanyanyasa mabingwa wa 1988 wa Tanzania Bara, Coastal Union FC Uwanja wa Taifa jijini hapa jana ikiwa ni hat-trick yake ya tatu Ligi Kuu ya Bara tangu aanze kukipiga Tanzania msimu uliopita.
Ilikuwa mara ya pili kwa mshambuliaji huyo pia kufunga mabao manne pekee yake katika mechi moja baada ya kufanya hivyo pia katika ushindi wa mabao 6-0 wa Simba dhidi ya Mgambo Shooting Stars Uwanja wa Taifa jijini hapa msimu uliopita.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top