Featured
Loading...

Kesi ya IPTL Dhidi ya Zitto Kabwe kusuluhishwa Machi 23 Kwa Siri


Mahakama Kuu inatarajia kusuluhisha kesi iliyofunguliwa na Kampuni ya Kufua Umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) dhidi ya Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe na wenzake Machi 23, mwaka huu.

Kesi hiyo namba 175 ya mwaka 2014 ilipangiwa kuanza kufanyiwa usuluhishi jana mbele ya Jaji Salvatory Bongole, lakini ilishindikana kutokana na upande wa walalamikaji ambao ni IPTL kushindwa kufika mahakamani.

Hata hivyo, Kaimu Msajili wa Mahakama hiyo Kitengo cha Usuluhishi, Beda Nyaki alisema kesi hiyo itasikilizwa kwa siri baina ya pande hizo.

“Kesi hii haiwezi kuripotiwa kwenye vyombo vya habari kwa sababu ipo katika hatua za kwanza za usuluhishi, hivyo kitu kitakachoongolewa baina ya walalamikaji na walalamikiwa kitakuwa ni siri yao,” alieleza Nyaki.

Alisema kusikilizwa kwa faragha kwa kesi hiyo ni hatua ya kupunguza gharama na muda.

Katika kesi hiyo, Kampuni za IPTL, Pan Africa Power Solutions (T) Limited na Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni hizo, Harbinder Sing Seth walifungua madai ya Sh500 bilioni dhidi ya Zitto, Mhariri wa gazeti la Raia Mwema, Kampuni ya Raia Mwema na Kampuni ya Flint Graphics ikiwa fidia kwa kuwakashfu kuhusiana na sakata la uchotwaji wa zaidi ya Sh300 bilioni katika Akaunti ya Tegeta Escrow.

Mawakili wanaomtetea Zitto ni Wakili Ntemi Masanja na Ivone Sianga ambao walidai kuwa walalamikaji walishindwa kufika mahakamani hapo na kusababisha kuahirishwa kwa kesi.

Ilidaiwa kuwa walalamikaji hao walichukua hatua ya kufungua kesi hiyo kufuatia makala aliyoyaandika Zitto katika gazeti la Raia Mwema la Agosti 13, 2014 katika ukurasa wa saba na wa 14, ikiwa na kichwa cha habari “Fedha za IPTL ni mali ya umma.’’

Walalamikaji hao walidai kuwa makala hiyo ni ya upotoshaji na ilikuwa na lengo la kuwachafua mbele ya jamii.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top