Featured
Loading...

Deni la Taifa Laongezeka Mara Dufu, Upinzani Washtuka Wataka CAG Kufanya Ukaguzi


DENI la taifa limeongezeka maradufu, hali ambayo imeifanya kambi Rasmi ya Upinzani kushtuka na kumtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kufanya ukaguzi maalum.

Ongezeko hilo, kwa mujibu wa kambi ya upinzani, deni hilo limeongezeka kwa kiasi hivyo, kutoka mwaka 2010 hadi mwaka jana.

Akiwasilisha maoni ya Kambi ya Upinzani kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Kwanza wa Maendeleo ya Taifa wa Mwaka 2011/12 hadi 2015/16 na mwelekeo wa Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa Mwaka 2015/16 hadi 2020/21, Naibu Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Wizara ya Fedha na Mipango, David Silinde, alisema hali ya deni la taifa inatisha na Bunge linapaswa kushituka.

Silinde alisema nchi itafilisika kama Ugiriki ikiwa Bunge halitachukua hatua madhubuti za kuisimamia serikali.

Alisema deni la taifa limekuwa na kufikia dola za Marekani bilioni 19.141 (Sh. trilioni 41.536). Alisema deni liliongezeka maradufu mwaka jana, baada ya serikali kukopa dola bilioni 3.846 (Sh. trilioni 8.347).

"Mwishoni mwa Juni, 2010, jumla ya deni la Tanzania lilifikia dola bilioni 9.9 (Sh. trilioni 13.6) kulingana na thamani ya dola kipindi hicho). Miaka mitano baadaye deni limefikia Sh. trilioni 41.5, lazima Bunge tushituke," alisema Silinde.

"Fedha zilizokopwa kuanzia 2010 hadi 2015 zilifanyia miradi ipi ya maendeleo? Mikopo hii ina riba kiasi gani, tumeweka nini kama dhamana ya kupatiwa mikopo au ile minong'ono mitaani ya vitalu vya gesi?

"Mkopo mkubwa wa mwaka 2010 ambao ni sawa na asilimia 5.9 ya deni lote ulitumika kufanyia jambo gani? Fedha hizi zimetumika kugharamia miradi gani au ndiyo EPA ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015?

"Majibu ya maswali haya yatapatikana tu kama itafanyika 'Special Audit' ya deni la taifa. Mkopo huu ni hatari zaidi kama hautalipwa kwa wakati kwani riba itaongezeka maradufu na kuifanya nchi ifilisike.

"Kwa sababu hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani inamtaka CAG kufanya ukaguzi maalum wa deni la taifa na kuleta taarifa ya ukaguzi huo bungeni kwa ajili ya kujadiliwa,” aliongeza.

Serikali yakubali

Akizunguma na Nipashe nje ya ukumbi wa Bunge jana mchana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, alisema serikali iko tayari CAG afanye ukaguzi huo kwa kuwa fedha hizo zilitumika kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.

"Wizara yangu haina kipingamizi, CAG aje atukague. Deni la taifa lipo tangu kipindi cha uongozi wa (Mwalimu Julius) Nyerere. Tunakopa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Tutamwonyesha CAG miradi iliyotekelezwa," alisema.

Awali, akieleza kuhusu Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa Mwaka 2015/16 hadi 2020/21, Silinde alilitaka Bunge kutunga sheria ya utekelezaji wa mpango huo kwa maelezo kuwa bila kufanya hivyo hautatekelezeka kama uliopita.

Mbunge huyo wa Mbozi Magharibi (CHADEMA), alisema mpango uliopita, ulikuwa na lengo la kujenga barabara kwa kiwango cha lami Km 5,204 (kila mwaka Km 1,040.8) ndani ya miaka mitano, lakini zilizojengwa ni Km 2,775 (kila mwaka Km 555), sawa na asilimia 53 ya lengo.

"Mwalimu Nyerere aliondoka (madarakani) mwaka 1985, aliliachia Shirika la Ndege (ATCL) ndege 11, lakini kwa sasa linamiliki ndege 'zero' (sifuri), ilhali likiwa na wafanyakazi wengi wanaolipwa kodi za wananchi," alisema.

Kuhusu reli, Silinde alisema serikali iliweka lengo la kukarabati Km 2,707 kwa kiwango cha 'standard gauge', lakini hadi sasa imekarabati Km 136 tu (wastani wa Km 27.2 kwa mwaka). Ili kutimiza malengo ya miaka mitano ya Km 2707, Silinde alisema serikali itatumia miaka 99.5.

Kweye kilimo, Silinde mpango uliopita ulikuwa na lengo la kukuza kilimo kwa asilimia sita kwa mwaka, lakini sekta hiyo imekuwa kwa asilimia 3.4 kwa kipindi chote cha miaka mitano, huku akidokeza kuwa mpango huo haukuleta matokeo chanya katika sekta ya elimu.

Kadhalika, katika mpango uliopita, Silinde alisema lengo lilikuwa kuzalisha Megawati 2,780 za umeme ndani ya miaka mitano, lakini katika kipindi chote zimeongezeka MW 496.24, hivyo Tanzania itahitaji miaka 13 kufikia malengo ya mpango wa kwanza.

Source: Nipashe

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top