Featured
Loading...

RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 32 na 33


Mtunzi:ENEA FAIDY

.... Shule ya sekondari Mabango ilikuwa na utulivu wa hali ya juu tangu Doreen alipoondoka shuleni pale. Licha ya kwamba kulikuwa na upungufu wa walimu lakini hali ilikuwa shwari kabisa. Wanafunzi waliendelea na masomo yao kama kawaida huku wakimshukuru Mungu kwa kuwaondolea mbaya wao aliyeisumbua shule ndani ya muda mfupi tu.

Majira ya saa saba mchana katika shule ile alifika Mwanaume mmoja wa makamo akiwa ameambatana na  mwanamke mmoja mwembamba mrefu. Wanafunzi wa shule waliokuwa karibu waliweza kugundua kuwa mwanamke yule bila shaka alikuwa ni mama yake Dorice kwa jinsi walivyofanana.  Nadia Joseph aliyekuwa anapita eneo lile la ofisi aliwasalimia kwa heshima kisha akasimama kidogo huku akitafakari jambo alilotaka kuzungumza.
"Samahani mama.. We ni ndugu yake Dorice.." Aliuliza Nadia huku akitabasamu.

"Ndio.. Ni mama yake mzazi.." Alijibu mama yule.
"Oh mmefanana sana... Vipi lakini hajambo?" Aliuliza Nadia akiwa anatabasamu lakini swali lile lilikuwa kama mwiba mkali moyoni mwa Mama Dorice kwani ujio wake pale shuleni ilikuwa ni kumfuata Dorice na kupata taarifa zake kwani ulipita muda mrefu sana bila mawasiliano yoyote.
"Kwani Dorice hayupo hapa shule?" Aliuliza Mwanaume aliyeambatana na Mama Dorice kwa mshangao. Na huyo alikuwa ni mjomba wa Dorice.

"Ah! Unataka kuniambia hayupo nyumbani?" Alishangaa Nadia lakini ndani ya muda mfupi alitokea madam Amina eneo lile hivyo Nadia aliamua kuondoka ili kukwepa adhabu.
Madam Amina aliwasogelea wageni wale na kuwasalimu. Kisha akawakaribisha ofisini. Bila kuchelewa wageni wale waliambatana na Mwalimu Na kuingia ofisini.
"Karibuni sana.. "
"Asante.. Sisi ni wazazi wa Dorice na tumekuja hapa kuuliza binti yetu anaendeleaje?"
"Dorice.. Alikuwa kidato cha nne?" Aliuliza mwalimu.
"Ndio!"

"Mmh! Mbona aliacha shule na tuliwapigia simu mkasema amefika"  alisema Mwalimu  Amina kwa mshangao. Kauli ile iliularua moyo wa mama Dorice na kumfanya achanganyikiwe sana, maana hakuna simu aliyopigiwa wala Kuambiwa chochote kuhusu mwanae.
"We mwalimu umechanganyikiwa? Mbona kama hujielewi eti?" Mama yule wa kinyaturu aliinuka kitini na kuanza kumfokea mwalimu.
Mwalim Amina aliamua kujitetea kwani hali ya hewa ilianza kuchafuka ofisini mle. "Tunamtaka mwanetu.. Mmemtorosha nyie? Au mmemuua?" Alizidi kucharuka mama Dorice.

Mwalimu Amina alikumbuka mbali, akakumbuka siku ambayo Dorice alipotea kisha wakapewa taarifa za upotevu wa mwanafunzi huyo. Barua ya maelezo iliandikwa kisha walimu wakapiga simu kwa wazazi wa Dorice. Lakini kwa bahati mbaya sana simu ilipokelewa na  jini Mansoor kwa namna ya ajabu sana. Na jini huyo aliongea sauti ya Mama Dorice na kuwafanya walimu wajiaminishe vizuri kuwa waliongea na mama Dorice lakini kumbe haikuwa hivyo na hakuna aliyejua siri hiyo zaidi ya Mansoor pekee.

"Mama tena nilipiga simu Mimi.. Na ulikubali mwanao aache shule.." Alijitetea madam Amina lakini hakueleweka.
Wazazi wa Dorice waliondoka kwa hasira sana shuleni pale huku wakiwa hawajui binti yao alienda wapi. Roho iliwauma sana lakini hawakuwa na jinsi. Waliondoka na gari yao waliokuwa wamekodi ikawafikisha kituo cha mabasi Iringa mjini.
 
Walishuka ili watafute sehemu ya kula chakula kwani hawakula chochote tangu asubuhi kisha wakate tiketi, ghafla kwa mbali sana Mama Dorice alimwona msichana kama Dorice. Alijifuta macho yake na kutazama vizuri akamtazama vizuri binti yule.
"Kaka Dorice yule pale"
"Yuko wapi?" Kaka yake alishtuka sana.
"Pale mbele kwenye watu wengi.. Tumfate haraka.." Alisema Mama Dorice akiwa tayari ameanza kupiga hatua kuelekea kule alipo msichana yule.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top