Featured
Loading...

Godbless Lema ampongeza Rais Magufuli.....Amshauri Awaangalie na Waliokaa Mahabusu Muda Mrefu

Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Godbless Lema amempongeza Rais John Magufuli kwa kutoa msamaha kwa wafungwa.

Pia, amemshauri kuwaangalia mahabusu waliokaa muda mrefu gerezani pasipo kupata haki.

Katika maadhimisho ya uhuru wa Tanganyika (Tanzania Bara)  Jumamosi Desemba 9,2017mkoani Dodoma, Rais Magufuli alitoa msamaha kwa wafungwa 8,157 kati yao 1,828 waliachiwa huru kuanzia siku hiyo.

Rais John Magufuli jana Jumapili Desemba 10,2017 ametia saini nyaraka za msamaha alioutoa kwa wafungwa 61 waliohukumiwa kunyongwa hadi kufa na wawili Nguza Viking na Johnson Nguza (Papii Kocha) waliohukumiwa kifungo cha maisha jela.

Msamaha huo umeonekana kumgusa Lema ambaye ni Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi. Lema   amesema kuna mateso wanayopata mahabusu ambayo yanahitaji kuangaliwa.

“Rais Magufuli, Mungu akubariki kwa msamaha uliotoa jana kwa wafungwa na hasa wale waliokaa magereza muda mrefu pamoja na wazee, msamaha ni ibada,” amesema Lema ambaye pia ni mbunge wa Arusha Mjini (Chadema).

“Ni msamaha muhimu kwao, mtu aliyehukumiwa maisha au kifo akipata msamaha ni jambo jema sana, ninafurahi wamesamehewa sasa hawatakuwa tena magereza maisha yao yote,” 

“Nimefurahi kwamba hata wale waliokuwa wamehukumiwa kunyongwa hasa wazee pia wamepata msamaha, kwangu ninaona ni jambo jema na zuri, kwa mtu anayejua huzuni ya magereza atakubaliana nami.”

Kuhusu mahabusu, Lema amesema, ‘’Wako mahabusu wamekuwa magereza kwa muda mrefu bila kesi zao kukamilika. Mheshimiwa  Rais fuatilia watu kama hawa pia.”

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top