Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imesema itatumia zaidi ya Sh1.2 bilioni
kwa maadhimisho ya miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar ambayo kilele chake
kitakuwa Januari 12 mwakani.
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud Mohamed amesema
hayo leo Jumapili Desemba 24,2017 ofisini kwake Vuga mjini Unguja
alipotoa taarifa ya maandalizi ya sherehe hizo.
Amesema
fedha hizo zinatarajiwa kutumika katika maandalizi ya siku ya kilele,
ufunguzi wa miradi 49 ya maendeleo ya kiuchumi, miradi ya maji, majengo
ya shule, umeme na barabara.
Waziri
amesema miradi 33 itazinduliwa baada ya kukamilika na 16 itawekwa mawe
ya msingi. Miradi hiyo ni ya taasisi za umma, jamii na ya wawekezaji.
Waziri
Mohamed amesema Serikali imepiga hatua katika kufanikisha huduma za
kijamii na maendeleo sambamba na lengo la Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka
1964.
Amesema
wananchi wanapaswa kujitokeza kuunga mkono jitihada za Serikali katika
kufanikisha maadhimisho hayo ambayo yatazinduliwa Desemba 30,2017 kwa
kufanya usafi wa mazingira.
Katibu
Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Dk Idriss Muslim Hijja amesema
miradi iliyopendekezwa kuingizwa katika maadhimisho imefuatiliwa na
kutolewa taarifa kwa sekretarieti ya halmashauri ya sherehe na
maadhimisho ya kitaifa.
Amesema
katika uzinduzi na uwekaji wa mawe ya msingi ya miradi, viongozi wa
kitaifa wa Serikali zote mbili wamejumuishwa wakiwemo marais, mawaziri
na wastaafu wa pande zote mbili.
Kilele
cha maadhimisho hayo kitakuwa Januari 12,2018 katika Uwanja wa Amani
mjini Unguja ambako Rais Ali Mohammed Shein atakuwa mgeni rasmi.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )