Featured
Loading...

Wanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Wazungumzia Sakata la Hosteli Yao Mpya Kuanza Kubomoka

Baadhi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wameingia hofu baada ya mabweni wanayoishi kuwa na nyufa.

Mabweni hayo yanayotumiwa na wavulana katika jengo la Block A yana nyufa sehemu mbalimbali kuanzia chini hadi ghorofa ya tatu.

Mbunge wa serikali ya wanafunzi (Daruso), Simon Masenga amesema nyufa hizo zilianza kuonekana wiki mbili zilizopita.

Amesema walitoa taarifa kwa meneja wa hosteli lakini majibu waliyopewa ni kuwa majengo hayo yako chini ya Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).

Mbunge mwingine wa serikali ya wanafunzi, Kumbusho Dawson amesema leo Jumatatu Desemba 4,2017 kuwa majengo hayo yana upungufu, ukiwemo wa maji kutuama kwenye bafu na kutokuwa na makabati.

"Tumelalamika kwa meneja wa mabweni kuhusu upungufu katika majengo haya na majibu tunayopewa ni kuwa bado yako chini ya TBA," amesema Dawson.

Majengo hayo yaliyojengwa na TBA kwa miezi minane yakielezwa kugharimu Sh10 bilioni yalizinduliwa Aprili 15,2017.

Ujenzi ulifanyika ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli la kumaliza tatizo la malazi kwa wanafunzi wa UDSM.

Picha zinazoonyesha nyufa kwenye majengo hayo zilianza kusambaa mitandaoni jana Jumapili Desemba 3,2017.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top