Waziri
wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamis Kigwangalla, amefanya ziara ya
kushtukiza katika bandari ya Dar es Salaam ambapo alibaini uwepo wa
makontena yenye magogo ambayo ni mazao ya misitu yaliyokaa bandarini
hapo kwa zaidi ya miaka 10.
Waziri Kigwangalla ameagiza Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii atangaze kujitokeza kwa wamiliki wa magogo hayo 938 na kama wamiliki wasipojitokeza, magogo hayo yatakuwa mali ya Serikali.
Aidha
Dkt. Kigwangalla ametoa siku 30 kwa wamiliki wa makontena 55
yanayodaiwa kuingizwa nchini kutoka nchini Zambia kujitokeza na
kuwasilisha nyaraka zao zenye kuthibitisha kama kweli yalivunwa nchini
Zambia na yalivunwa wapi na kwa vibali gani vya nchi hiyo pamoja na
kufuatilia nyaraka za kuingiza ndani ya Tanzania.
Ameagiza
kitengo cha kuzuia ujangili kifuatilie kubaini uhalisia na uhalali wa
taarifa hizo vinginevyo yatakuwa mali ya Serikali.
Dkt.
Kigwangalla amefanya ziara ya kushtukiza bandarini hapo kufuatia uwepo
wa taarifa za uvunaji holela wa magogo nchini, ambapo kuna taarifa kuwa
kuna wafanyabiashara wa kigeni wanagawa vifaa vya kuvunia bure kwa ahadi
ya kuuziwa mzigo na wahusika, pia uwepo wa taarifa kwamba kuna baadhi
ya watumishi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) wanaotoa
vibali na kugonga nembo kinyume cha taratibu za kisheria, hali
inayotishia usalama wa raslimali adimu ya misitu yetu ya asili.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )