Featured
Loading...

Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF) Latoa Tamko Zito Kuhusiana Na Hali Ilivyo Kwa Sasa Zanzibar



Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF) limetoa tamko kuhusiana na hali ilivyo sasa Zanzibar likisema linafadhaishwa na kusikitishwa nayo na kwamba linaamini isingefikia hapo endapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ingechukua hatua katika kutatua mgogoro huo. 
Katika tamko hilo lililosambazwa kwenye vyombo vya habari jana baada ya kikao cha TCF juzi, yamo mapendekezo manne likiwamo la kuitaka Serikali kurejesha mchakato wa Katiba kwa kuzingatia maudhui yaliyomo katika Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba ili kuondoa utata wa Serikali kushiriki masuala ya Zanzibar. 
“Sisi viongozi wa dini tuliokutana leo tarehe 15.03.2016, tunafadhaishwa na kusikitishwa na hali ya Zanzibar kwa sasa.
"Hali ya Zanzibar isingefika hapo ilipo iwapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ingechukua hatua ya kutatua mgogoro huu.
"Hali hii ya Zanzibar na udhaifu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano vinapelekea kushindwa kwa Serikali ya Muungano kuchukua hatua ya kusaidia hali ya Zanzibar. Hata hivyo, udhaifu huu wa Katiba hauondoi wajibu wa Serikali ya Muungano kuhakikisha haki na amani vinatawala Zanzibar,” ilisema sehemu ta tamko hilo lililotiwa saini na Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Mwanza, Jude Ruwa’ichi.
Jukwaa halikufafanua hali ya Zanzibar kwa sasa inay- osababisha maaskofu hao kufadhaika lakini huenda limekusudia kueleza hofu iliyotanda katika visiwa hivyo tangu Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ilipofuta uchaguzi na matokeo yote ya uchaguzi wa Zanzibar, na baadaye kutangaza kuwa utarudiwa Machi 20. 
Vyama tisa kikiwamo Chama cha Wananchi (CUF) vilitangaza kujitoa lakini ZEC imesisitiza vyama vyote vitashiriki. 
Hali imeendelea kuwa tete na hivi karibuni yamekuwapo matukio ya uchomaji moto makazi ya watu katika visiwa hivyo yanayoonyesha uvunjifu wa amani kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa marudio Jumapili ijayo. 
Baadhi ya matukio hayo ni kuchomwa moto maskani za CCM na CUF, nyumba 11 za watu ikiwamo ya Kamishna wa Polisi Zanzibar, Hamdan Omar Makame iliyoko Kijichi, Mkoa wa Mjini Magharibi. 
Baada ya kutathimini hali hiyo, TCF imesema pamoja na udhaifu wa Katiba, Serikali ya Muungano bado ina wajibu wa kuhakikisha uhuru, haki na amani vinatawala Zanzibar kuelekea uchaguzi huo wa marudio.
 “Hata hivyo, Serikali ya Muungano pamoja na taasisi zinazosimamia mchakato wa uchaguzi, zinao wajibu wa kuhakikisha kuwa suala la uhuru, haki na amani Zanzibar vinalindwa na kuheshimiwa. Suala la uhuru, haki ni wajibu wetu sisi viongozi wa dini na Watanzania wote na halina mbadala,” ilisema sehemu ya tamko hilo. 
Jukwaa limesisitiza kwamba ni jukumu la kila mmoja kutimiza wajibu wake kulinda uhuru, haki na amani na kuweka uzalendo kwanza kuliko kutanguliza maslahi binafsi au ya vyama vya siasa. 
Mbali ya pendekezo la kuitaka Serikali kurejesha mchakato wa Katiba, pia limewataka viongozi wa dini kuwahimiza Watanzania wote kuendelea kuiombea Tanzania (Bara na Zanzibar) ibaki kuwa Taifa lililojengwa katika msingi ya uhuru, haki na amani. 
Pili, limelitaka Jeshi la Polisi, vikosi vya ulinzi na usalama na Jeshi la Wananchi wa Tanzania, kwa wakati huu kuendelea kutimiza wajibu wa kusimamia amani na taratibu kwa haki bila upendeleo.
 Mwisho limesisitiza kwamba viongozi wa dini wabaki kuwa sauti ya kinabii na wahubiri wa uhuru, haki na amani wakati huu, wakati wa uchaguzi na haada ya uchaguzi.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top