Featured
Loading...

Flashback: Zanzibar 1989!- Watumbatu Walinishangaza Sana...!


    Ndugu zangu,
    Kabla ya kwenda Zanzibar kwa mara ya kwanza mwaka 1989, nilisoma habari nyingi za kihistoria juu ya watu wa visiwa hivyo. Nilisoma pia historia ya mapinduzi yao ya mwaka 1964.
    Nakumbuka nilisafiri na jahazi lililojengwa kwa mbao liitwalo Ras Nungwi. Safari ilichukua saa nane majini, maana jahazi lilijaza shehena kubwa ya magunia ya chumvi.
    Enzi hizo Zanzibar jahazi halikufika mpaka kwenye gari kutia nanga. Tulisubiri mbali na gatini na ikaja mitumbwi midogo kutuchukua abiria. Ilikuwa ni kuurukia mtumbwi kutoka jahazini. Ukiuokosa na kuangukia majini, basi, ni lazima uogelee!
    Basi, nikiwa kisiwani Unguja nikatamani nifike kisiwa kidogo cha Tumbatu. Kutoka Mikokotoni Unguja hakuna umbali mrefu kufika Tumbatu kwa mtumbwi.
    Ni kisiwa kidogo chenye urefu wa takribani kilomita nane, na mapana ya kilomita mbili. Niliwaona Watumbatu wakiwa tofauti sana na Waunguja.
    Watumbatu, kwa mtazamo wangu hata wa wakati huo nikiwa kijana mdogo sana, niliwaona kuwa ni watu wenye usiri mkubwa. Kwanza walionekana kushangaa iweje kijana mdogo kutoka bara na wala si Unguja nimekwenda kutaka kujua habari zao.
    Na ugumu ukawa pia kwangu kufahamu wanachoongea, waliongea labda niseme Kibantu cha Kitumbatu. Niliwaelewa, lakini kwa tabu.
    Hata wakati huo, Watumbatu walionyesha kuwa wao ni tofauti na Waunguja, kwamba Tumbatu ni ya Watumbatu. Hawakutaka kuyazungumzia sana ya Unguja, na waliona kuwa ni mbali na kwao, hata kama ni umbali wa kilomita kadhaa tu.
    Kwa mashaka, Watumbatu walinikaribisha makwao na hata chakula na maji ya kunywa. Muda mwingi nilihisi wakinihofia , kuwa ni mtu niliyetumwa jambo kwao.
    Mwishowe, wanawake wa Kitumbatu ni warembo sana, as'kwambie mtu..!
    Maggid, (P.T)

    Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
    © Copyright MZALENDO HURU
    Back To Top