Featured
Loading...

Darasa la saba wafeli hesabu za la Darasa pili

Wanafunzi wa darasa la saba wameshindwa kufanya hesabu za darasa la pili baada ya kubainika ni asilimia 69 pekee wanaoweza kufanya hesabu hizo. Pia asilimia 48 tu ya darasa la tatu  wanaweza kufanya hesabu za darasa la pili

Aidha, asilimia 38 ya wanafunzi wa darasa la tatu ndiyo wanaoweza kusoma hadithi ya kingereza ya darasa la pili na asilimia 82 ya wanafunzi wa darasa la saba wamebainika kuweza  kusoma hadithi ya Kiingereza ya darasa la pili.

Utafiti huo kwa mujibu wa taasisi ya Twaweza ulifanyika katika wilaya 159 ukishirikisha sampuli ya watoto 112,455 wenye miaka kati ya saba hadi 16.

Akizindua ripoti hiyo jana Desemba 3 katika shule ya msingi mazoezi afisa tawala wilaya ya Monduli, Sharif Mziray alisema kwamba serikali imeipokea ripoti hiyo kwa mikono miwili na imewasaidia kuwafungua mambo mengi.

Mziray, alisema  kwamba serikali inaichukulia ripoti hiyo kama changamoto na kuanzia sasa watatengeneza mazingira wezeshi kwa walimu na wanafunzi ili kujenga mazingira bora ya watoto kujifunza.

“Hii ni changamoto kwetu sisi kama serikali ya wilaya lakini wazazi pamoja na walimu mna changamoto ya kuhakikisha mnaweka mazingira mazuri ya watoto kujifunza”alisema Mziray

Hata hivyo, mratibu wa programu ya Uwezo wilayani Monduli, Mohammed Nkinde alisema  kwamba wilaya hiyo imeshika nafasi ya 43 kati ya 159 katika ngazi ya kitaifa na nafasi ya 4 katika ngazi ya mkoa  katika uwezo wa watoto kujifunza.

Nkinde, alisema kwamba mahudhurio ya walimu na ufundishaji kwa ujumla upo chini wilayani Monduli kwa kuwa kiwango cha mahudhurio wilayani humo kinaonyesha kuwa ni asilimia 86 ya mahudhurio ya walimu na asilimia 75 ya mahudhurio ya wanafunzi kiwango ambacho hakiridhishi.

“Hii inaonyesha kwamba muda wa wanafunzi na mwalimu kukutana au kufundisha darasani wakati wa muda wa shule ni mdogo na hivyo wanafunzi hawapati muda unaopaswa kufundishwa ili waweze kujifunza stadi za msingi” alisema  Nkinde

Ofisa maadili na nidhamu kutoka tume ya utumishi wa walimu wilayani humo, Rhoda Msemo alikemea tabia ya baadhi ya wazazi ambao hawakubahatika kwenda shule kutokagua madaftari ya watoto wao na kusema tabia hiyo haifai.

“Kuna baadhi ya wazazi hawakupata bahati ya kwenda shule hivyo wanawaogopa watoto wao hata kukagua home work (kazi za nyumbani) hawakagui hii si sawa kagueni kazi zao hawa watoto msiwaogope” alisema Msemo

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top