Featured
Loading...

Baba Mzazi wa Mo Dewji Afunguka Alivyompata Mwanaye....Amshukuru Rais Magufuli

Familia ya bilionea Mohammed Dewji, imesimulia namna kijana wao alivyoachiwa na watekaji usiku wa kuamkia leo.

Baba yake mzazi Gullam Dewji Hussein ameviambia vyombo vya habari kuw alipigiwa simu leo alfajiri Oktoba 20, 2018 akielezwa kuwa mwanae amepatikana.

Gullam amesema alijulishwa kuwa mwanaye amepatikana akiwa katika gari ambalo lilitelekezwa katika viwanja vya Gymkhana jijini hapa.

Amesema Mo Dewji baada ya kushushwa katika gari hilo alitembea kutafuta msaada wa simu.

Amebainisha kuwa baada ya kupokea simu hiyo alifika haraka eneo la tukio na kufanikiwa kumuona mwanaye.

“Namshukuru Mungu nimemkuta Mo akiwa salama na haraka nilimpeleka nyumbani lakini tumemkuta ana majeraha kidogo ila jambo la kushukuru ni kwamba yuko hai,” amesema Gullam.

“Tulipofika nyumbani tulianza kufanya mawasiliano na Jeshi la Polisi kwa kuwapa taarifa kuwa kijana wangu nimempata na wao (polisi) walifika nyumbani kwangu Oysterbay.”

Gullam amemshukuru Rais John Magufuli kwa kufanikisha kupatikana kwa mwanaye.

Mo alitekwa saa 11 alfajiri ya Oktoba 11 mwaka huu, katika hotel ya Colosseum iliyoko Oysterbay jijini Dar es Salaam, alipokwenda kufanya mazoezi.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top