Wafanyakazi
 watano wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (Nemc) 
wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka 
sita ya uhujumu uchumi, ikiwamo kula njama na kughushi saini ya Waziri 
wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Januari 
Makamba.
Washtakiwa
 hao wamesomewa mashtaka hayo jana Jumatano Oktoba 31, 2018 na wakili wa
 Serikali, Faraja Nguka mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Augustina 
Mmbando.
Akisoma
 mashtaka hayo, Nguka alidai washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka 
sita ikiwamo la kula njama, mawili ya kughushi, kuwasilisha nyaraka ya 
uongo, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kusababisha hasara ya 
Sh 160 milioni.
Wakati
 washtakiwa hao wakisomewa mashtaka hayo,  mshtakiwa mwenzao, ofisa 
mazingira wa Nemc, Magori Wambura (38) ambaye hakuwepo mahakamani, 
imetolewa hati ya kumkamata ili asomewe mashtaka yanayowakabili wenzake.
Washtakiwa
 waliosomewa mashtaka ni ofisa mazingira wa Nemc, Deusdith Katwale (38) 
mkazi wa Ubungo Msewe, mtaalam wa Tehama, Luciana Lawi (33) mkazi wa 
Ubungo Msewe, sekretari wa baraza hilo, Edna Lutanjuka (51) mkazi wa 
Mbezi Beach St Gasper, msaidizi wa ofisa Mwaruka Mwaruka (42) mkazi wa 
Ukonga Mombasa na ofisa mazingira NEMC, Lilian Laizer (27) mkazi wa 
Ukonga Mombasa.
Washtakiwa
 hao kwa pamoja wanadaiwa  kati ya Septemba  27, 2016 na April Mosi, 
2018 Dar es Salaam walikula njama ya kutenda kosa la kughushi.
Katika
 shtaka la pili washtakiwa hao wanadaiwa kuwa  Oktoba 17, 2017 Dar es 
Salaam kwa udanganyifu walighushi cheti cha tathmini ya uharibifu wa 
mazingira chenye namba ya usajili EC/EIA/3366 wakijaribu kuonyesha kuwa 
cheti hicho ni halali na kwamba kimetolewa na Nemc wakati wakijua si 
kweli.
Katika
 shtaka la tatu wanadaiwa kuwa Oktoba, 2017 Dar es Salaam kwa nia ovu 
walighushi saini ya Makamba katika cheti cha tathmini ya uharibifu wa 
mazingira chenye usajili namba EC/ EIA/3366 wakijaribu kuonyesha kuwa 
cheti hicho ni halali na kimetolewa na Nemc wakati wakijua si kweli.
Katika
 shtaka la nne,  mshtakiwa Edna anadaiwa kuwa Oktoba  2017 katika ofisi 
za Nemc Makao Makuu Dar es Salaam kwa kujua alitoa cheti cha kughushi 
cha tathmini ya uharibifu wa mazingira chenye namba ya usajili 
EC/EIA/3366 cha Oktoba 17, 2017 kwa Deogratius Chacha, akijaribu 
kuonyesha kuwa cheti hicho ni halali na kimetolewa na Nemc wakati akijua
 si kweli.
Katika
 shtaka la tano, washtakiwa hao wote wanadaiwa kuwa kati ya Septemba 27 
na Aprili 6 ,2018 walijipatia kwa njia ya udanganyifu Sh160 milioni toka
 kwa PMM Estate (2001) Ltd kwa madai kuwa wangeweza kufanya tathmini ya 
uharibifu wa mazingira na kumpatia cheti ambacho kinatolewa na Nemc 
kitendo ambacho si kweli.
Katika
 shtaka la sita washtakiwa hao wanadaiwa kuwa kati ya Septemba27, 2016 
na Aprili 6, 2018 Dar es Salaam waliisababishia Nemc hasara ya Sh160 
milioni.
Baada
 ya kusomewa mashtaka hayo, washtakiwa hao hawakuruhusiwa kuongea 
chochote kwa sababu mashtaka ya uhujumu uchumi Mahakama ya Kisutu haina 
mamlaka ya kuisikiliza hadi Mahakama Kuu.
Washtakiwa wamepelekwa rumande na kesi hiyo imeahirishwa hadi Novemba 14, 2018.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
 

 
 
 
 
 
 
 
