Featured
Loading...

Baada ya Okwi Kuvunja Mkataba Denmark,Simba Wamfanyia Mapango Aje Kucheza Mechi ya Yanga..!!


 
UONGOZI wa Simba umesema unafanya mpango wa kumrejesha kikosini mshambuliaji wake wa zamani Emmanuel Okwi aliyevunja mkataba na klabu ya Sonderjyske ya Denmark.
Taarifa za kwenye mtandao wa klabu hiyo juzi ziliandika kwamba Okwi amefikia makubaliano ya kuvunja mkataba baada ya kukosa nafasi ya kucheza kwenye kikosi hicho.
Jana jioni Ofisa habari wa Simba, Haji Manara aliandika kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii: “Kocha Omog (Joseph- kocha mkuu wa Simba) ikimpendeza, Emmanuel Okwinho (Okwi) dimbani Feb 18, hiyo ndio habari mpasuko, ukinuna ongeza limao,”.
Simba inatarajia kucheza na Yanga katika mechi ya raundi ya pili ya Ligi Kuu baada ya kutoka sare ya bao 1-1 katika mechi ya kwanza.
Alipoulizwa  kuhusu taarifa hizo, Manara alikiri kuwa uongozi wake uko kwenye mchakato wa kumnasa mchezaji huyo na ikiwezekana atumike kwenye mechi zilizosalia za Ligi Kuu.
“Ni kweli tutamsajili kama mchezaji huru,” alisema.
Hata hivyo, tayari dirisha dogo la usajili kwa klabu za ligi limeshafungwa mpaka msimu ujao. Akilizungumzia hilo, ofisa habari wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas alisema Simba haiwezi kumtumia Okwi kwa sababu dirisha la usajili limeshafungwa.
“Ingewezekana kama usajili wa dirisha dogo ungekuwa haujafungwa, lakini dirisha limeshafungwa hivyo kama wanataka kumtumia, wasubiri mpaka usajili mwingine,” alisema.
Wakati wa usajili wa dirisha dogo Desemba mwaka jana Simba ilitaka kumsajili mshambuliaji huyo Mganda lakini ilishindwa baada ya klabu ya Sonderjyske kutaka ilipwe karibu sh milioni 240.
Hasimu wa Simba, Yanga pia ilijaribu kutaka kusajili mshambuliaji mwingine ili ashindane na Donald Ngoma baada ya kudaiwa kugoma kucheza kwenye mechi za kombe la Mapinduzi lakini ilishindikana kwa vile dirisha la usajili lilishafungwa.
Sonderjyske ilimsajili Okwi Julai 2015 kutoka Simba kwa mkataba wa miaka mitano uliotakiwa kumalizika mwaka 2020 ambapo tangu amesajiliwa Okwi alicheza mechi nne tu za Ligi Kuu ya Denmark na mbili za kombe la DBU ambapo alifunga mabao mawili.
Simba pia iliwahi kumuuza Okwi Etoile du Sahel ya Tunisia mwaka 2013 kwa dola za Marekani 300,000 kabla ya kusajiliwa na Yanga alipocheza kwa muda mfupi na kurejea Simba.
Okwi ni mshambuliaji kipenzi cha wanasimba kutokana na mafanikio aliyoipatia timu hiyo ambapo jana baada ya Manara kuweka suala lake kwenye mitandao ya kijamii, karibu mashabiki wengi wa soka walikuwa wakimzungumzia.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top