Featured
Loading...

Godbless Lema Awakumbuka Wafungwa....Amuomba Rais Magufuli Aingilie Kati la Wakili Mwale

Leo  ikiwa ni sikukuu ya Krismasi, Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Godbless Lema amewatakia kheri wafungwa na mahabusu nchini.

Lema ambaye pia ni mbunge wa Arusha Mjini (Chadema) katika salamu alizotoa jana Jumapili Desemba 24,2017 amekumbusha kilichomtokea sikukuu ya Krismasi mwaka jana akitaka wenye mamlaka kusimamia haki kwa weledi.

‘’Wakati ninawakumbuka na kuwatakia heri ya Krismasi mahabusu na wafungwa wote nchini ni muhimu watu wote mlioko kwenye vyombo vya sheria mjue wajibu wenu, unapokosa utu na upendo maana yake ni kuumiza watu na kutesa watu mahali fulani,” amesema Lema.

Amesema, “Krismasi mwaka jana nilikuwa nimeshikiliwa kama mahabusu Gereza Kuu Arusha kwa kunyimwa dhamana, tukiwa gerezani mimi na wenzangu tulikuwa tunaandaa sikukuu ya Krismasi.”

Lema amesema anawakumbuka rafiki zake wengi aliokaa nao vizuri ambao wengine wamefungwa na baadhi bado wako mahabusu.

“Kwa kweli zaidi namkumbuka sana wakili Median Mwale ambaye amekuwa mahabusu kwa kipindi cha zaidi ya miaka sita. Ninamuomba Rais aingilie kati suala la Mwale, kwa kweli huyu mtu inatosha kuwepo magereza kwa zaidi ya miaka sita bila kuhukumiwa. DPP najua unajua watu wengi wako magereza, nguvu uliyopewa na sheria inapokosa upendo basi nguvu hiyo inakuwa ni ukatili,” amesema Lema.

Amesema Krismasi mwaka jana alikuwa gerezani baada ya ibada iliyoongozwa na Askofu Lebulu (Josephat - Askofu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha) walifanya maandalizi ya kula chakula ambacho familia zao  ziliwapelekea.

“Tukiwa tunakula wakili Mwale alisema, Lema wewe utatoka na mimi na wenzangu namuomba Mungu Krismasi inayokuja niweze kuwa nje, kwa bahati mbaya wakili Mwale na rafiki zake bado wameshikiliwa gerezani.”

Amesema kwa kipindi alichokuwa gerezani ameelewa huzuni za familia na watuhumiwa, ndiyo sababu Rais alipowasamehe wafungwa na hasa wenye makosa makubwa alimshukuru kwa sababu anajua huzuni ya kukosa uhuru.

Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )
© Copyright MZALENDO HURU
Back To Top