Leo
ikiwa ni sikukuu ya Krismasi, Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi,
Godbless Lema amewatakia kheri wafungwa na mahabusu nchini.
Lema
ambaye pia ni mbunge wa Arusha Mjini (Chadema) katika salamu alizotoa
jana Jumapili Desemba 24,2017 amekumbusha kilichomtokea sikukuu ya
Krismasi mwaka jana akitaka wenye mamlaka kusimamia haki kwa weledi.
‘’Wakati
ninawakumbuka na kuwatakia heri ya Krismasi mahabusu na wafungwa wote
nchini ni muhimu watu wote mlioko kwenye vyombo vya sheria mjue wajibu
wenu, unapokosa utu na upendo maana yake ni kuumiza watu na kutesa watu
mahali fulani,” amesema Lema.
Amesema,
“Krismasi mwaka jana nilikuwa nimeshikiliwa kama mahabusu Gereza Kuu
Arusha kwa kunyimwa dhamana, tukiwa gerezani mimi na wenzangu tulikuwa
tunaandaa sikukuu ya Krismasi.”
Lema amesema anawakumbuka rafiki zake wengi aliokaa nao vizuri ambao wengine wamefungwa na baadhi bado wako mahabusu.
“Kwa
kweli zaidi namkumbuka sana wakili Median Mwale ambaye amekuwa mahabusu
kwa kipindi cha zaidi ya miaka sita. Ninamuomba Rais aingilie kati
suala la Mwale, kwa kweli huyu mtu inatosha kuwepo magereza kwa zaidi ya
miaka sita bila kuhukumiwa. DPP najua unajua watu wengi wako magereza,
nguvu uliyopewa na sheria inapokosa upendo basi nguvu hiyo inakuwa ni
ukatili,” amesema Lema.
Amesema
Krismasi mwaka jana alikuwa gerezani baada ya ibada iliyoongozwa na
Askofu Lebulu (Josephat - Askofu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha) walifanya
maandalizi ya kula chakula ambacho familia zao ziliwapelekea.
“Tukiwa
tunakula wakili Mwale alisema, Lema wewe utatoka na mimi na wenzangu
namuomba Mungu Krismasi inayokuja niweze kuwa nje, kwa bahati mbaya
wakili Mwale na rafiki zake bado wameshikiliwa gerezani.”
Amesema
kwa kipindi alichokuwa gerezani ameelewa huzuni za familia na
watuhumiwa, ndiyo sababu Rais alipowasamehe wafungwa na hasa wenye
makosa makubwa alimshukuru kwa sababu anajua huzuni ya kukosa uhuru.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )